Featured post

KASISI FISADI : LUSAKA AZOMEWA BUNGOMA

 Wanyeji wa Bungoma wamemkemea Gavana wa Jimbo hilo Kenneth Makelo Lusaka. Katika maoni waliyotoa mtandaoni, wananchi wamempaka samli ya ufi...

Tuesday, 19 March 2019

MABALOZI WA SERA

Wametugeuza nzi, matatizo hawaoni
Wasokuwa na mapenzi,mwatuona hawayawani
Hawasikii ukwenzi, wana nta sikioni
Mabalozi wake sera, wamezika zao sera

Habari magazetini, wajifanya hawasomi
Na picha mitandaoni, hawaoni asilani
Matangazo redioni, hawajui zasemani
Mabalozi wake sera, wamezika zao sera

Kila siku vikaoni, waketi wakijadili
Na vinyuaji mezani, wakikagua faili
Wanapofika mwishoni, midia hawaikabili
Mabalozi wake sera, wamezika zao sera

Maji yakikosekana, kwao hilo hawajali
Watasimama bayana, wakitenga hela kweli
Hatimaye wanakana, na kuilaani hali
Mabalozi wake sera, wamezika zao sera

Njaa inapovamiza, nchi kule kaskazi
Wajifanya wanakaza, sura bandia za kazi
Vilio wanavipaza, na hawatoi machozi
Mabalozi wake sera, wamezika zao sera

Wananchi wakilia, turkana na Baringo
Ufisadi watwambia, kugeuza zetu shingo
Lao ni kututania, wakideka kwa maringo
Mabalozi wake sera, wamezika zao sera

Na vyakula magalani, vinaoza twaambiwa
Nazo hela mabenkini, zinazidi kuibiwa
Na mnyonge masikini, kwa njaa anauliwa
Mabalozi wake sera, wamezika zao sera

Mirefu yao midomo, hawaishi majigambo
Mwetu shida zilizomo, waziona vijimambo
Waiba bila ukomo, wakiboboja umombo
Mabalozi wake sera, wamezika zao sera

Matozi yamenitoka, yamenilovya machoni
Nazo nguvu zanitoka, kwa ulodumu uhuni
Kaka Si'wa naodoka, nikikemea shetwani
Mabalozi wake sera, wamezika zao sera




No comments:

Post a Comment