Wanasema waneni kuwa elimu haina mwisho. Ni kweli kwamba
binadamu haiachi elimu hata akiwa kaburini kwani huko,hujifundisha jinsi ya
kuwa mpweke,kupambana na joto na mafunza makubwa makubwa na kuishi gizani.
Elimu ni kweli haina mwisho kwani katika kila hatua anayopiga binadamu, kutoka
tumboni mwa mamake,akaja duniani kwa kilio cha kubadilika kwa mazingira,akakuzwa
kwenye maisha ya tamu chungu hadi kufikia kiwango cha kuolewa au kuoa. Hapo
akarambishwa asali na shubiri ya maisha ya ndoa. Katika hatua zote
hizo,binadamu huyu hujifunza jinsi ya kupeta mtama na kutenganisha mchele na
dume ili angalau ajisawazishe na maisha ya humu duniani. Anajielimisha. Lakini
hiyo ni elimu inayofungamana na methali ya elimu maisha si vitabu. Elimumaisha
ambayo mtu hahitaji kutahiniwa darasani na matokeo yake kupewa. Elimumaisha ni
ile inayohitaji uelekezi na matokeo yake mara nyingi hutegemea mtazamo wa mtu
binafsi kimaisha. Elimumaisha haina mwisho. Lakini elimu vitabu je!
Hadhi ya masomo humu nchini inaendelea kudidimia na karibuni
yataonekana kama ‘zilizopendwa’ kutokana na mkondo ambao elimu ya vitabu
imechukua. Tuanzie kule chini ambapo wanafunzi wengi hupewa mafundisho
yanayolenga kupita mtihani bali si kuoanisha ajifunzayo yeye na mazingira ya
kihalisia. Kwa mtazamo huu,mwanafunzi hubeba ile dhana ya kupasi mtihani hadi
shule za upili. Elimumaisha hujichopeka ndani kutokana na mabadiliko ya
mazingira ambapo badala ya mwanafunzi kuchagua majibu kama ilivyokuwa awali,
inampasa ajieleze moja kwa moja. Hapa,elimumaisha huchuja tiara na ndege. Na
mara nyingi,kwa kuwa wengi huazimia kuwa ndege,watatumia mbinu zote ili
kuhakikisha kuwa jongoo anapanda mtungi. Wizi wa mtihani huchukua nafasi kubwa
katika akili za mwanafunzi. Ajabu ni kuwa walimu pia husaidia katika vitendo
hivi haramu kwa kisingizio cha; huenda mtama mui,wapishi pia wakatwikwa ubaya.
Hapa elimu vitabu,shabaha yake kuu hubadilishwa na kumfanya mtu aasi mipaka ya elimumaisha na kumfanya awe
mwewe wa kuotea vifaranga kwa jicho lake kali hata akiwa amefukiwa kwa mavumbi
kule angani. Muradi mwenye kuku awe amezubaa au hayupo kabisa. Mwalimu naye
hutoa machozi ya mamba au tuseme huwa jogoo wa ‘uta wangu u kuleee’ ilhali
bayana anaifahamu.
Kwa kujaribu kuoanisha mwanga na giza,wanafunzi hawa
hujipata vyuoni wakifanya kozi ambazo alama zao zinawaruhusu ila ndani
moyoni,wao hujua kuwa asilani, ng’ombe hawi mbogo. Hili husababisha kubadilisha
kozi na ambapo kozi zinazositiri manusura wa kwingineko ni zile zinazohusisha
elimu na ualimu kwa jumla.
Mambo yakiwa msagunda mara tena,mtindo wa kula ugali kwa uma
au niseme kumeza vidonge vya dawa kwa sharubati huendelea badala ya maji
kulingana na masharti ya mganga. Kwa kuogopa kunawa mikono, labda kwa
uzembe,woga wa maji au hata kuona kuwa ni kupoteza muda huko,ulama huchukua uma
kwa jina ‘mwakenya/ndula’ na kuitumia kula ugali ambao kwa shibe kamili,ya
kweli na inayojulikana kwa wafrika wengi,ni lazima ule kwa kuumega kwa viganja.
Baadaye,wao huhitimu na kuingia katika uwanja wa kusaka kazi.
Fikiria basi wafanyakazi ambao wataajiriwa baada ya tamthilia
ya wizi kutoka mimba kupasuka hadi kumaliza chuo kikuu. Fikiria utendakazi wao.
Fikiria kuhusu mwalimu ambaye alipitia katika njia hizo zote na akaajiriwa na
serikali kuja kumfunza mwanao. Atakuwa kielelzo kipi kwa atifali! Ikiwa gunia
la chumvi hurishai chumvi,basi usishangae kizazi kijacho kikiwa vile vile hadi
ujio wa yesu mnazareti. Zingatia Yule daktari wa karne ya ishirini na moja.
Hajali uzima wa mtu,hajali dhamani yake kwa nchi. Ameuzika utu kwenye kaburi na
kulitandazia zege. Kwake,maisha na matibabu si haki kwa makabwela. Pesa bora.
Fikiria kuhusu mhandisi yule,labda ndiyo sababu ya kupenda sana wachina na
wajapani kwa kuwa labda mpanda hila,ni sharti avune ufukara.
Ukimpata matiang’i mwambie,
Mtoto memnyang’anya kisuche,
Hata banzi asimpe
Kampokeze ombwe……labda hilo litafanya mti ufe,shinale na
tanzuze zikauke.
No comments:
Post a Comment